Friday, June 29, 2012

MGOMO WA MADAKTARI

MGOMO WA MADAKTARI

Serikali yafanya
maamuzi mazito

* Wagonjwa waliotelekezwa Muhimbili kutibiwa Lugalo

* Vigogo wizarani, madaktari wastaafu kuingia kazini

SERIKALI imetangaza kutumia Hospitali ya Jeshi Lugalo badala ya Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) ambayo madaktari wake wameingia kwenye mgomo.

Hatua hiyo imelenga kusaidia kutibu wagonjwa wenye hali mbaya hususan wakati huu wa mgomo, pia madaktari wastaafu na wale waliopo wizarani wameombwa kusaidia kutoa huduma katika hospitali mbalimbali.

“Tunajaribu kuona uwezekano wa utaratibu utakaowezesha madaktari wastaafu na wale waliopo wizarani kurudi kusaidia kutoa huduma kwa sasa,” alisema Waziri Mkuu Mizengo Pinda.

Waziri Mkuu Pinda aliyasema hayo bungeni jana, wakati akijibu maswali ya papo kwa papo na kufafanua kwamba hali ya matibabu katika hospitali mbalimbali ikiwemo MNH ni tete kutokana na mgomo wa madaktari.

Alisema wakati serikali inaendelea kuzungumza na madaktari ili warejee kazini, imeona ni bora kuwaomba madaktari wastaafu na wale wa wizarani kusaidia kuhudumia wagonjwa.

Waziri Mkuu alisema pia serikali imeiomba Hospitali ya Lugalo, kusaidia kutibu wagonjwa na hospitali zake ndogo ndogo.

AHUZUNISHWA NA YA ULIMBOKA

Akizungumzia tukio la kutekwa na kupigwa kwa Mwenyekiti wa Jumuia ya Madaktari Tanzania, Dk. Steven Ulimboka, Pinda alisema serikali aihusiki kwa namna yeyote na tukio hilo.

Alisema Ulimboka alishirikiana vyema na serikali katika masuala ya kutatua mgogoro huo, hivyo hakukuwa na mpango wa serikali kumdhuru.

Waziri Mkuu Pinda alisema amesikitishwa na kitendo hicho na anamuombea kwa Mungu ili aweze kupona haraka kwani walikuwa wakienda naye vizuri katika kutafuta suluhu ya mgomo wa madaktari.

Hata hivyo, alisema kutokana na taarifa alizopewa, tukio hilo linahitaji uchunguzi wa kina na ufanywe haraka ili ukweli wa jambo hilo uweze kubainika.

"Mazingira ya tukio hili yana utata mwingi, yanahitaji uchunguzi wa kina kwa kwa sasa kila mmoja anahisia zake wengine wanasema serikali wengine hivi. Kwa upande wangu nasema kama ni serikali basi itakuwa ni watu wa ajabu sana kwa sababu Dk. Ulimboka tulikuwa wote mpaka tumefika mahakamani na vyombo vyote vinajua sasa kidogo inanipa taabu kama ni serikali inataka kufanya hivyo ili iweje,’’ alihoji.

“Njia rahisi tusubiri uchunguzi wa kina na mimi jana (Juzi) nimeagiza wakamilishe uchunguzi huo haraka," alifafanua Pinda.

Sambamba na hilo, alisema serikali haiwezi kutoa kauli juu ya mgomo huo kama ilivyohaidi bungeni juzi na badala yake inasubiri maamuzi ya mahakama kutokama kuahirishwa kwa kesi hiyo.

Kuhusu kauli yake, aliyoitoa kwamba ‘liwalo na liwe’ alisema haikuwa na maana kama ambavyo wengi wanafikiria.

Kimsingi alisema kauli hiyo, ililenga kuingilia suala hilo hata kama lipo mahakamani na si vinginevyo.

Waziri Mkuu Pinda alitoa ufafanuzi huo, wakati akijibu swali la Kiongozi wa Kambi ya Upinzani, Freeman Mbowe ( Hai – CHADEMA), aliyetaka kujua ukweli kuhusu kauli hiyo kama inahusiana na tukio la kutekwa na kupigwa kwa Ulimboka.

CCM YALAANI

Katika hatua nyingine, Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimelaani kitendo cha kikatili cha kutekwa na kujeruhiwa kwa Dk. Ulimboka.

Kutokana na hilo, kimeitaka serikali kufanya uchunguzi wa kina na wa haraka kuwabaini waliohusika ili wachukuliwe hatua za kisheria.

Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema hayo jana na kusisitiza kuwa CCM inalaani vikali kitendo hicho kwa kuwa kinakiuka haki za binadamu.

"CCM imesikitishwa na kitendo hicho cha kinyama na kimeitaka serikali kufanya uchunguzi wa kina ili kuwabaini watuhumiwa," alisema Nape.

Alisema tukio la kutekwa na kujeruhiwa kwa Dk.Ulimboka na watu wasiojulikana linapaswa kufuatiliwa kwa karibu na vyombo vya usalama ili hatua zichukuliwe dhidi ya waliohusika.

Dk.Ulimboka alitekwa usiku wa kuamkia juzi na watu wasiojulikana ambao walimkamata na kumbeba kwenye gari jeusi lisilo na namba za usajili.

Watekaji hao walimpiga na kumjeruhi sehemu mbalimbali za mwili wake na kumtupa katika msitu ulioko eneo la Mambwepande ambako aliokotwa na wasamaria wema akiwa taabani.

Kufuatia tukio hilo, Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, imeunda jopo la wapelelezi linaloongozwa na Mkuu wa Upelelezi wa Kanda hiyo, Ahmed Msangi kuchunguza tukio hilo.

BARAZA LA USALAMA LAKUTANA

Baraza la Usalama la Taifa, litajadili hali ya usalama ikiwemo wimbi la ujambazi ili hatua za haraka zichukuliwe.

Akijibu maswali ya papo kwa papo jana, Waziri Mkuu Pinda, alisema kumekuwa na matukio ya ujambazi ambayo yameanza kutisha hapa nchini ikiwemo lile la Serengeti.

“Ni kweli yapo matukio ambayo yamejitokeza ambayo yameanza kutupa wasiwasi likiwemo la Serengeti,” alisema.

Alisema Rais Jakaya Kikwete alikuwepo mjini Dodoma juzi na amerudi Dar es Salaam kwenda kuzungumzia masuala hayo.

Alisema baada ya baraza hilo la usalama kujadili litatoa maelekezo ya kina yatakaoweza kudhibiti hali hiyo.

Alikuwa akijibu swali la Said Nkumba (Sikonge –CCM), aliyetaka kujua serikali inachukua hatua gani dhidi ya kuibuka upya kwa ujambazi katika maeneo mbalimbali.

Nkumba alitoa mfano wa tukio la kuuawa kwa watalii Serengeti, kupigwa kwa kiongozi wa madaktari Dk. Ulimboka na usalama wa mipaka kutokana na vifo vya raia wa Ethiopia katika msitu wa Kongwa mkoani Dodoma.

Pia, Waziri Mkuu Pinda alisema Tanzania Bara haitakuwa na kinyongo kama Zanzibar itafanikiwa kupata mafuta.

Alisema maamuzi ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuamua kusimamia suala hilo yenyewe haina matatizo.

“Kwangu kama Zanzibar ikiweza kupata mafuta naona Tanzania Bara hatutakosa kitu chochote kwani faida mojawapo ni kuwa Bara sasa itapata mafuta pua na mdomo,” alisema Pinda.

Alikuwa akijibu swali la Khatibu Saidi Haji, aliyetaka kujua nini kauli ya serikali juu ya uchimbaji wa mafuta.

Katika hatua nyingine, Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) nayo imelaani kitendo cha kupigwa na kujeruhiwa kwa Dk. Ulimboka.

Mwenyekiti wa tume hiyo, Jaji mstaafu, Amir Manento, alitoa tamkoa la kulaani tukio hilo jana mjini Dar es Salaam na kuwa imesikitishwa na kitendo hicho.

Alisema kitendo hicho cha kinyama kinakwenda kinyume na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 kifungu cha 12(2), kinachoitaka jamii kutambua na kuthamini utu wa mtu.

Jaji Manento alisema Tanzania ni nchi yenye amani na inayofuata sheria na taratibu zake, hivyo kwa sababu yoyote ile ni kosa kumteka na kumtendea mtu vitendo vya kinyama na vya udhalilishaji wa utu wake.

No comments: