Thursday, June 14, 2012

BAADA YA KUSAFIRI NA TRENI

Fagio la Mwakyembe

lamkumba mtumishi TRL

*Aagiza afukuzwe kazi mara moja

*Amnasa akitoza nauli isiyo halali

*Abaini madudu chungu tele

NA THEODOS MGOMBA,DODOMA

WAZIRI wa Uchukuzi Dk. Harrison Mwakyembe, amemuagiza Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Reli Tanzania (TRL), kumfukuza kazi mmoja wa wafanyakazi wa shirika hilo kwa kumtoza mmoja wa abiria nauli ya kubwa.
Dk. Mwakyembe aliyasema hayo jana asubuhi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, baada ya kuwasili mjini hapa kwa treni kutoka Dar es Salaam.
Waziri huyo, alisema amegundua madudu mengi yanayofanywa na wafanyakazi wa kampuni hiyo dhidi ya abiria, baada ya kusafiri na treni hiyo.
Alisema mmoja wa watumishi wa kampuni hiyo bila kumtaja jina, alimtoza abiria fedha nyingi ya mizigo, huku akimpa stakabadhi inayoonyesha kiwango tofauti na alicholipa.
Dk. Mwakyembe alisema vitendo vya ulanguzi wa tiketi kwa abiria na rushwa toka kwa watumishi wa kampuni hiyo, vimekithiri.
“Nimetembelea behewa moja hadi jingine, nimeyaona mambo mengi ikiwemo uchakavu wa mabehewa na nimezungumza na abiria wameniambia mambo mengi ya kusikitisha,’’ alisema.
“Ndani ya treni hii, hakuna tofauti kati ya ‘First Class na Third Class’, yaani daraja kwa kwanza na la tatu yote hovyo tu,” alisema Waziri huyo.
Waziri Dk. Mwakyembe ambaye aliwasili mjini hapa saa 1.30 asubuhi jana akitokea jijini Dar es Salaam, alisema inashangaza kuona abiria wakilipishwa fedha kwa ajili ya mizigo yao kinyume na sheria.

“Abiria mmoja amelipishwa Sh. 25,000, lakini amenikabidhi stakabadhi ambayo imeandikwa sh. 9,000 tu, huu ni wizi,’’ alisema.
Alisema kufuatia madudu hayo, ameuagiza uongozi wa TRL kumbaini mtu huyo mara moja ili hatua za kinidhamu zikuchukuliwe dhidi yake.
Kero nyingine aliyoishuhudia ni watoto wa miaka mitatu kukatiwa tiketi ya mtu mzima wakati si sahihi.
“Naahidi na nitahakikisha napambana nao wale wote wasioitakia mema treni yetu na kubwa ninawaomba hata wabunge sasa watumie usafiri huu ili waweze kujenga hoja nzuri bungeni,” alisema.
Dk. Mwakyembe alisema kuanzia Desemba mwaka huu, serikali kupitia wizara yake, imejipanga kuhakikisha wanarudisha safari za reli kati ya Dar es Salaam na Mwanza hadi Mpanda kama ilivyokuwa awali.

No comments: