Monday, July 23, 2012


Watumishi sita MV Skagit mbaroni

JESHI la Polisi Zanzibar linawashikilia wafanyakazi sita wa meli ya MV Skagit akiwemo mmiliki wake Saidi Abdulrahman pamoja na nahodha wa meli hiyo, Mussa Makame Mussa, wanahojiwa na polisi.


Watuhumiwa hao walikuwa wakihojiwa katika Ofisi za Upelelezi Makao Makuu ya Jeshi la Polisi mjini Zanzibar ambapo Naibu Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai Zanzibar, ACP Yusuph Ilembo, amesema watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani kujibu mashtaka yanayowakabili.

Kamanda Ilembo amesema kuwa makachero wa polisi wanaendelea na uchunguzi na kutafuta taarifa nyingine zinazohusiana na tukio hilo.

Hata hivyo, nahodha wa zamu siku ya tukio hilo la kupinduka na kuzama kwa meli hiyo ya MV Skagit, Mussa Makame Mussa, ameelezea kwa ufupi jinsi ajali hiyo ilivyotokea na namna yeye alivyonusurika.

Alisema ajali hiyo ilitokea baada ya kupigwa na dhoruba na mawimbi yaliyoambatana na upepo mkali, ambapo yeye alinusurika kufa maji baada ya kuruka kwa kutumia mlango wa mbele wa meli hiyo na kuanza kuogelea ambapo alijichanganya pamoja na abiria wengine walionusurika na kuokolewa na vyombo vya uokozi.

Wakati huohuo, wapiga mbizi wa vikosi vya ulinzi na usalama leo wamefanikiwa kuzipata maiti nyingine tano akiwemo mwanamke mmoja na wanaume wanne.
Katika upekuzi wa maiti hizo, makachero wa polisi walibaini kitambulicho cha kupigia kura kutoka kwa mmoja wa marehemu kilichokuwa na jina la Philip John Busiya aliyezaliwa mwaka 1977 katika kijiji cha Mapilinga, kata ya Igokelo, wilaya ya Misungwi, mkoani Mwanza.

Kupatikana kwa miili hiyo, kunaifanya idadi ya maiti kufikia 73. Maiti nyingine 68 zilipatikana siku za mwanzo baada ya kutokea kwa ajali hiyo ambapo kati ya hizo, maiti 54 zilitambuliwa na kuchukuliwa na ndugu na jamaa kwa ajili ya mazishi.

Maiti hiyo iliyopewa namba 72, pamoja na maiti nyingine nne, zimezikwa katika makaburi ya pamoja ya Kama yaliyoko nje kidogo ya mji wa Zanzibar.

Eneo hilo la Kama pia lilitumika kwa kuwazika watu wengine waliokosa ndugu wakati wa ajali ya meli ya Spice Islander iliyotokea Septemba 9, 2011.

Kupatikana kwa miili hiyo kumetokana na juhudi zinazoendelea kwa kuvishirikisha vikosi vya ulinzi na usalama, wazamiaji wa makampuni binafsi pamoja na Mamlaka ya Bandari Zanzibar wakati wakiwa katika harakati za kuitafuta boti hiyo ili kuweza kubaini kama kuna miili mingine iliyosalia kwenye meli hiyo chini ya bahari.

Aidha, juhudi za kutaka kuiibua meli hiyo zinaendelea ambapo wazamiaji wa JWTZ, polisi, KMKM, JKU, Bandari na wale wa makampuni binafsi na wale wa kujitegemea wakiendelea na kazi ya kutafuta mahali ilipo meli hiyo ili kuona kama wataweza kupata miili mingine iliyonasa kwenye vyumba vya meli hiyo ambayo imekokotwa na maji kutoka eneo ilipozama.


...Uokoaji waelekea ukingoni

UOKOAJI wa watu na miili ya waliopoteza maisha katika ajali ya meli ya Mv Skagit unaelekea ukingoni, huku tukio hilo likizidi kugonga vichwa vya Watanzania.

Hadi sasa hakuna jibu la moja kwa moja kubainisha sababu ya ajali hiyo. Serikali imeahidi kuunda tume kuichunguza, ingawa hata tume za namna hiyo zilizoundwa awali kutokana na ajali kama hii, hazijatoa majibu sahihi kwa wananchi.

Katika ajali hiyo miili ya watu 70 hadi juzi ilikuwa imeopolewa, 140 waliokolewa wakiwa hai wengine zaidi ya 100 hawajulikani walipo. Hata hivyo, idadi kamili ya abiria waliokuwa kwenye meli hiyo mpaka sasa ni kitendawili kutokana na uzembe na mfumo mbovu wa kutambua idadi ya abiria wanaosafiri katika vyombo kadhaa.

Suala la utata katika idadi ya abiria wa meli, boti au treni limeendelea kuwa tatizo sawa na donda ndugu ambalo kwa miaka mingi halifanyiwi kazi.

Hata kwenye meli iliyozama katika Bahari ya Hindi mwishoni mwa mwaka jana na ile ya MV Bukoba iliyozama katika Ziwa Victoria Mei 21, 1996 tatizo hilo lilijitokeza na halikufanyiwa kazi.

Mfano, katika ajali ya Mv Bukoba iliyokuwa na uwezo wa kubeba abiria 400, hadi leo haijulikani ilizama na abiria wangapi. Baadhi wanataja zaidi ya 600, wengine zaidi ya 800, lakini idadi ya vifo vilivyosajiliwa katika Ofisi ya Vizazi na Vifo Wilaya ya Mwanza wakati huo ni 1,024.

Leo tumelazimika kuzihoji mamlaka zinazohusika, Sumatra na ZMA kwamba, kwa nini zimeshindwa kuweka utaratibu wa kufahamu idadi ya abiria wanaokuwamo kwenye vyombo vya usafiri na hasa vinavyosimamiwa kwa sheria za ndani na za kimataifa?

Ingawa hadi sasa hakuna taarifa rasmi kuhusu tatizo la meli ya Skagit, inafahamika kuwa imesajiliwa na Mamlaka ya Usafiri Baharini Zanzibar (ZMA) na kupewa cheti cha ubora, kuanzia Agosti 24, 2011 kinachomalizika Agosti 24, 2012.

Pia tunatambua kuwa, ingawa Sumatra inajivua suala la usajili, meli hiyo inatakiwa kukaguliwa kila inaporuhusiwa kuelea katika maji ya Tanzania Bara, kama utaratibu ulivyo kwa meli zote za Tanzania au zilizopata cheti cha usajili wa meli za kimataifa.

Kwa jumla, ajali hii ina mambo mengi ya kujiuliza, mojawapo likiwa sababu za sheria ya ZMA, kuruhusu usajili wa meli bila ukomo wa umri wake (open registry). Hivi sheria hiyo ilitungwa kwa masilahi ya nani? Je, hawakuona kama ni sheria ya kuifanya nchi yetu kuwa dampo la vyuma chakavu?

Je, waliotunga sheria hii hawakuona umuhimu wa kuweka ukomo wa umri kama ilivyo kwa Sumatra ambayo hairuhusiwi kusajili meli yenye umri zaidi ya miaka 20? Maswali yote yanabainisha umuhimu wa kupitia upya sheria za vyombo hivi na usimamizi ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

No comments: